Tuesday, May 30, 2017

SIASA IONDOLEWE KWENYE MIKATABA


Na Elias Mhegera Mjadala mkubwa unaoendelea nchini Tanzania kwa sasa ni kuhusu yaliyojiri kuhusiana na ‘mchanga’ wa dhahabu au ‘makinikia’ na pia athari zake baadaye kisiasa na kisheria pia. Watanzania wamechachamaa kwa hamasa kubwa, wakiwashambulia wabunge wao kwa kuruhusu mambo ya aina hii yaendelee kwa muda mrefu kwa sababu za kulindana na kutumia wingi wa wale waliokuwa wanaunga mkono. Wadau mbali mbali wanapendekeza kwamba mikataba yote ya madini ijadiliwe upya. Lakini pia wanataka sheria za mikataba zizingatiwe ili taifa ingie matatani na wawekezaji Wananchi kwa ujumla wanaona kwamba kuna miswaada ilipitishwa kwa hati ya dharura ka malengo mabaya. Na haya yote yaliwezekana kwa sababu ya mfumo mbovu wa kisiasa. Mjadala wa jambo hili ni mpana ipo ya kisheria, na kisiasa pia. Prof. Abdallah Safari ambaye ni wakili wa kujitegemea pamoja na kwamba yeye pia ni makamu mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) anasema hili ni janga jingine. Anaiona hofu kwamba uamuzi uliochukuliwa hata kama una manufaa kisiasa lakini unaweza kuwa na athari za kisheria. Sababu kubwa ni kwamba mikataba hii ilifikiwa kwa maridhiano ya pande mbili. Na kwa maana hiyo pande hizo zinaweza kuirejea mikataba hiyo na kuangalia wapi pa kurekebishwa. Anahofu kwamba upo uwezekano kwamba wawekezaji wakienda mahakamani yanaweza kujitokeza yale yale ya ile kesi ya ‘samaki wa Magufuli’ kama ilivyotambulishwa wakati ule. Anasema Tanzania inayo bahati kwamba ipo sheria ya mikataba inayoheshimika kimataifa inayoitwa “The Nyerere Doctrine of State Succession” ambayo ilihusu mikataba iliyokuwapo wakati wa uhuru na mabadiliko yaliyotakiwa kufanyika baada ya nchi kupata uhuru. Prof. Safari anasema kwamba ameongea na wakili Ibrahim Bendera aliyekuwa wakili wa walalamikaji katika kesi ya meli na wakili huyo anasema kwamba mwisho wa jambo hili ni kufikishwa kwenye mahakama za kimataifa na serikali yetu inaweza kuingia matatani. Wakili maarufu wa kujitegemea jijini Mwanza Bw. James Njelwa ambaye pia amewahi kufanya kazi na asasi ya sheria za mazingira (LEAT) anasema kwamba huwezi kusema tu kwamba sheria imevunjwa bila kuwa umeusoma mkataba wenyewe ulikuwa na vipengele gani. Hata hivyo hofu yake ni kwamba iwapo mliingia mkataba na mwenzako huwezi kuuvunja mkataba huo kwa kutumia jeshi la Polisi au kwenda na vyombo vya habari katika kuuvunja. Hofu yake ni kwamba wawekezaji wanaweza kujiona kwamba labda walidhalilishwa kwa mambo hayo kuhusisha sana vyombo vya habari. Kimsingi mikataba hiyo ilifikiwa chini ya utawala wa awamu ya tatu chini ya Rais Benjamin Mkapa. Hofu ni kwamba ripoti ya Prof. Abdulkarim Mruma itaibua mambo mengi ya tokea 1998 nchi ilipoingia mikataba hii. Na kwa mana hiyo wapo wanaoona kwamba Prof. Sospeter Muhongo hakustahili kubebeshwa mzigo wa lawama yeye peke yake na watendeji wengine walioadhibiwa bali hata marais wastaafu Mkapa na Jakaya kikwete. Wadau wanaona sheria zilikuwa zinampa wakati mgumu Prof. Muhongo kufanya lolote ila kutii alichokikuta kwa lengo la kuilinda nafasi yake ya uwaziri. Kamati ya Mh Rais iliyokuwa chini ya Prof Mruma inasema nchi ya Tanzania imeibiwa sana. Lakini mwekezaji(Acacia) anasema ripoti hiyo imeongopa,haijatoa takwimu za ukweli. Mwanasheria mkuu wa serikali wa zamani Andrew Chenge amenukuliwa na vyombo vya habari akisema kuwa kamati ya Rais iliyoongozwa na Prof Mruma, imeongopa kwa kutoa taarifa isiyo sahihi. Ni mazingira hayo yanayoleta sintofahamu ya kisaa na kisheria pia. Rais wa awamu ya nne Jakaya Kikwete na Rais John Magufuli wote wamefanya kazi katika awamu hizo mbili. Kulingana na utamaduni wa kiutendaji serikalini yapo mambo ambayo viongozi waliotangulia na waliopo madarakani wanaweza kuyamaliza kimya kimya. Jambo hilo linawezekana zaidi kwa serikali iliyoongozwa na chama kimoja kwa muda wote kama ilivyo kwa Chama Cha Mapinduzi (CCM). Mkataba huu mmoja unaopigiwa kelele sasa ni miongoni mwa mikataba mingi iliyowahusu viongozi wa kitaifa hususani rais mwenye dhamana kuu ya fedha za serikali yaani “sovereign bond”. Mkataba huu ni mmoja wa viashiria vya matumizi mabaya ya dhamana kwa malengo ya kujipatia utajiri kwa watu binafsi, kikundi cha watu na hata labda chama tawala chenyewe CCM. Kwa mantiki hiyo uamuzi huu unampa heshima kubwa mtu binafsi ambaye ni rais wa sasa na kwa wakati huo huo unawavunjia heshima watangulizi wake wawili Mzee Mkapa na mwenzake Kikwete. Ni vigumu sasa kubashiri athari za muda mrefu za kisiasa za jambo hili yaani mpambano wa kujijengea kuheshimika ‘fight of legacies’. Hata hivyo zinakidhi mahitaji ya sasa ya kisiasa. Ni kweli kwamba yanayofanywa na Rais Magufuli ni kiashiria cha uzalendo, lakini ni vyema pia kuwa na mkakati wa kuondosha ufisadi na uoza nchini bila kuvunja sheria. Wizi katika sekta ya madini haukuanza leo, na hata kelele dhidi ya wizi huo hazijaanza leo. Kujiuzulu au kuondolewa kwa waziri wa nishati na madini hakujaanza leo. Ni vyema kuja na mkakati wa kudumu wa kushughulikia suala hilo ‘comprehensive approach’ badala ya kuangalia leo bila kukumbuka kesho nini kinaweza kutokea. Kivita unaweza kusema Prof. Muhongo ni ‘cross fire victim’ yaani risasi zinarushwa kutoka upande mmoja kwenda mwingine na mtu asiyevifahamu vizuri vita hivyo anajikuta kapigwa risasi. Wakati wa Uchaguzi Mkuu wa 2015 CCM ilimuuza ‘mtu binafsi’ Magufuli kwa sababu chama kilihofu kwamba hakiuziki, kwa sasa mtu huyo anataka kuhalalisha kwa Watanzania kwamba kweli alistahili kuwa rais wa nchi na anayo mapenzi ya dhati kwa nchi na watu wake. Ni vigumu kwa watendaji walioko serikalini kufahamu wanatakiwa wafanye nini katika mazingira ya sasa wakati rais wa nchi amelenga kujenga utamaduni mpya. Mawaziri na watendaji wengine wanafahamu kwamba ili kulinda ajira yako ni lazima ufuate kanuni za mfumo wa serikali ulioukuta. Muhongo aliteuliwa na wanasiasa wanaoujua mfumo kuliko yeye ambaye muda mwingi alikuwa vyuoni na labda hata akiwa nje ya nchi. Kwake ilibidi ajue ajipange vipi ili aweze kukidhi mahitaji ya mfumo wa sasa bila kuwakera watangulizi ambao hasa ndiyo walianza kumuamini na kumkabidhi wadhifa. Na kwa mantiki hiyo Prof. Muhongo na hata wenzake waliodhibiwa amehukumiwa kwa kubeba dhambi ya watu wengine ambazo hata rais wa sasa alipata kuzibeba kwa kile kinachoitwa ‘collective responsibility’ yaani uwajibikaji wa pamoja akiwa ndani ya awamu hizo. Pamoja na kumpongeza Rais Magufuli kwa hatua zake madhubiti ni vyema pia akazikumbuka sheria za kimataifa ili taifa lisije kuingia matatani mbele ya safari. Tuwasiliane: mhegera@gmail.com Simu 0715-076272 Pichani: Mwanasheria Mkuu wa Serikali George Masaju

Friday, February 6, 2015

Asasi za kiraia zakerwa na misamaha ya kodi
Na Elias Mhegera                   Januari 23, 2015
Mtandao wa Kutetea Usawa Katika Kodi nchini Tanzania umesikitishwa na lindi la misamaha ya kodi nchini na kuziomba mamlaka husika kuachana na mtindo huo mara moja.
Akizungumza na blog ya Mfafanuzi, kwa niaba ya mtandao huo unaofahamika kwa jina la Tanzania Tax Justice Coalition kwa lugha ya Kiingereza, Mratibu wa asasi ya Policy Forum Bw. Semkae Kilonzo anasema mara nyingi kodi imekuwa ikiwaumiza wanyonge na kuwapatia unafuu mkubwa matajiri wakubwa.
Shirika la Policy Forum ndilo mwenyeji wa mtandao huo ambao unaundwa na wadau mbali mbali zikiwamo asasi za kiraia na wanahabari.
“Inasikitisha kuona kwamba bado serikali yetu inaendekeza misamaha mikubwa ya kodi wakati taifa lina hali mbaya kiuchumi, hospitali hazina dawa, shule hazina madawati na hata baadhi ya familia zina njaa,” anasema Kilonzo.
Kauli yake inakuja kufuatia taarifa zilizotolewa kwenye vyombo vya habari siku ya Jumanne juma lililopita baada ya Kamati ya Bunge ya Fedha za Umma kuelezwa kwamba kulikuwa na ongezeko la misamaha ya kodi kwa kiwango cha zaidi ya shilingi bilioni 340 katika Mwaka wa Fedha uliopita wa 2013/2014.
Akilizungumzia ongezeko hilo, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Bw. Rished Bade alisema baadhi ya misamaha hiyo ilitolewa kwa makampuni yanayochunguza uwepo wa mafuta na gesi asilia katika vina vikubwa vya bahari.
Alisema kwamba misamaha hiyo ilikuwa kiasi cha shilingi bilioni 1.48 katika mwaka fedha wa 2012/13 na ikapanda hadi 1.82 katika Mwaka wa Fedha 2013/2014 ambao uliishia tarehe 30, Juni 2014. Ongezeko hili ndilo limeleta malalamiko kutoka katika taasisi mbali mbali nchini.
Kupatikana kwa taarifa hiyo kulikuja katika shughuliza kawaida za kamati za Bunge, ambapo mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Zitto Kabwe aliwasomea mrejesho huo wanahabari waliokuwapo katika ofisi za Bunge jijini Dar es Salaam.
Akiizungmzia hali hiyo ofisini kwake Mikocheni kwa Warioba, Bw Kilonzo alisema Tanzania imekuwa ikiathiriwa na ukusanyaji wa kodi usiozingatia maadili. “Uwazi katika ukusanyaji wa kodi ni mojawapo ya mahitaji katika dhana nzima ya utawala bora,” alisema Bw. Kilonzo.

Anaongeza, “tunaishukuru serikali yetu kwa mipango ya kufanya mabadiliko katika kodi ya ongezeko la thamani, na jitihada za kupunguza misamaha ya kodi, lakini ni muhimu ihakikishe kwamba kila mmoja anachingia kwa usawa kulingana na kipato chake katika hazina ya taifa.” 
Alichukua fursa hiyo kulikumbusha Bunge la Tanzania kukamilisha Miswaada miwili yaani Mswaada wa Ongezeko la Thamani wa 2014, na Mswaada wa Utawala wa Kodi wa Mwaka 2014, anashauri miswada hiyo ijadiliwe haraka ili kuondoa maduku duku.
Akiuzungumzia wa kwanza anasema unalenga katika kubakiza misamaha katika maeneo muhimu tu baada ya kutolewa kwa cheti cha misamaha hiyo na Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), baada ya tathmini ya kina.
Bw. Kilonzo anasema ni kweli kwamba kutokana na makubaliano ya kidiplomasia katika mikataba ambayo pia Tanzania imeiridhia baadhi ya bidhaa za kidiplomasia hazitozwi kodi. Lakini bidhaa hizo ni zile zilizomo katika shughuli za kiserikali tu.
Anashauri kwamba mamlaka ya waziri wa fedha yapunguzwe au yadhibitiwe pale yanapohusika katika utoaji wa misamaha ya kodi kwa sababu kwa njia hiyo upo uwezekano mkubwa wa misamaha hiyo kutumiwa vibaya na hata wakati mwingine kuambatana na matumizi ya rushwa.
Kuhusu namna nyingine ya kupunguza misamaha ya kodi anashauri kwamba kuwepo na mjadala mpana wa kina unaowahusisha wadau mbali mbali badala ya serikali kuu kujimilikisha maamuzi yote yanayohusiana na kodi.
Zaidi ya hayo anasema wale wote wanaosamehewa kodi waripotiwe kwenye vyombo vya habari na sababu za misamaha hiyo ziwekwe bayana. “Sioni sababu ya usiri katika misamaha hiyo zaidi ya kunufaishana kwa wenye mamlaka,” anaonya.
Kuhusiana na Mswaada wa Utawala wa Kodi wa 2014, Kilonzo anasema iwapo Mswaada huo utapitishwa na kuwa sheria,  basi sheria hiyo italeta mapinduzi ya aina yake tokea kuanzishwa kwa mamlaka hiyo (TRA), mwaka 1995.
Anazungumzia uelewa wake katika masuala ya kodi kutokana na mafunzo aliyoyapata kutoka katika taasisi mbali mbali kama vile Tax Justice Network of Africa, Financial Transparency Coalition, Global Financial Integrity n.k. na kusema siku zote misamaha mingi ya kodi haina manufaa kwa walio wengi bali kwa makundi machache.
Akifafanua zaidi anasema wakati mwingine kodi imekuwa ikitumika kama nyenzo ya kisiasa kwa manufaa ya vyama tawala na wakati mwingine hata kwa lengo la kuwaumiza wafanya biashara wanaounga mkono vyama vya upinzani, na wafanya biashara wanaoonekana kwamba hawazuingi mkono serikali zao.
“Ni jukumu letu sisi asasi za kiraia kuelimisha umma kwamba si haki kwa serikali kutoa misamaha ya kodi kwa makubaliano ya nipe nikupe, yaani kuwasamehe kodi wafanyabiashara wanaovichangia vyama tawala, kodi ni mali ya wananchi wote si mali ya watawala,” anaonya.
Anasema kwamba hata katika Miswaada iliyopelekwa bungeni bado kuna vipengele vinavyompatia mamlaka ya mwisho Kamishna Mkuu wa TRA katika kutoa misamaha jambo ambalo bado linaweza kutumika vibaya.
Kilonzo anasema katika mazingira ya sasa Kamishna Mkuu wa TRA amekabidhiwa mamlaka makubwa sana ambayo yanaweza kutumika vibaya na wenye mamlaka hususani kwa matakwa ya kisiasa.
Anashauri kwamba hata hicho kinachoitwa kwamba ni misamaha kwa lengo la kuvutia uwekezaji nia lazima izingatie uwazi, uwajibikaji, na haki.
“Katika ujumla wake suala la utawala wa kodi linahitaji uwazi, maadili, na uwajibikaji siyo wa maafisa wachache wanaopokea amri kutoka serikalini bali wanaotimiza majukumu yao kutokana na mamlaka ya kitaasisi,” anahitimisha.

 Pichani: Kamishina Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania Bwana Rished Bade 

Wednesday, January 7, 2015

MJADALA WA AKAUNTI YA TEGETA ESCROW-MHARIRI EVARIST MWITUMBA USIPOTOSHWE!

Na Elias Mhegera
Kwanza naomba nikusalimie kwa jina la Bwana muumba wa mbingu na dunia, na kisha nikutakie heri ya mwaka mpya! Siku ya juzi niliona comments zako zikiunga mkono uchambuzi kuhusiana na sakata la akaunti ya Tegeta Escrow, sikuridhishwa na comments zako na ndiyo maana nimeandika hoja hizi.
Nikirejea katika mada yenyewe kuhusiana na sakata la akaunti hiyo, kwanza naomba nikiri kwamba kwa tabia yangu binafsi huwa sipendi sana malumbano, hususani na wanataaluma wenzangu katika jambo lolote lile.
Pili naomba nikiri kwamba na mimi nimekuwa nikisikia fununu kwamba miongoni mwa sababu za kukuzwa sana kwa sakata hili ni jaribio la ‘vigogo’ kadhaa kuandaa mazingira ili Prof. Sospeter Muhongo alinyakue jimbo la Wakili, na Mbunge wa Musoma Vijijini Mhe. Nimrod Mkono.
Inadaiwa kwamba Prof. Muhongo analindwa kwa nguvu zote kwa sababu ni mbabe na anaweza kuendelea kuwalinda vigogo waliohusika na ufisadi katika mikataba ya mafuta na gesi asilia, rejea sakata la Muhongo kuwalinda watendaji wa TPDC.
Tutakwenda mbela na kurudi nyuma, lakini jambo moja ni dhahiri, kuna ufisadi mkubwa unaowahusu viongozi wetu wakubwa, ambao sasa tunawataka wajimalize wao wenyewe! Soma dhana hiyo katika novel ya James Hadly Chase: You Find Him-I’ll Fix Him, hebu ichote hapa:file:///C:/Users/USER/Desktop/james-hadley-chase-you-find-him.pdf
Novel hii inaelezea jinsi ambavyo muovu anaaminika, na anatakiwa kuchukua hatua juu ya wale wanaoonekana kwamba ni ‘waovu’! ni dhahiri kwamba muovu huyo atajitahidi kuwalinda kwa nguvu zote kwani ndani ya nafsi yake anafahamu fika kwamba yeye ndiye kawaponza hao wanaoonekana kwamba ni waovu/wahalifu-hiyo ndiyo Escrow!
kutokana na maslahi mapana ya taifa, na pia mazingira yanayolizunguka sakata hilo mpaka sasa, nalazimika kutoa mchango wangu, tena kwa majonzi makubwa kwa sababu nalazimika kutaja mambo ambayo yatawagusa watu ambao kwangu siyo kwamba ni marafiki wa karibu bali wengine ni ndugu zangu wa damu.
Hata hivyo udugu wetu huo nisingependa unifunge mdomo wangu pale ninapoona kwamba madhara ya mimi kukaa kimya ni makubwa kulikoni kuyaweka wazi niyafahamuyo kwa manufaa na mustakabali wa taifa zima. Nimeisoma makala ya Kazi Msemakweli akiwatetea vilivyo maprofesa wawili, Sospter Muhongo na Anna Tibaijuka.

Agizo la Prof Tibaijuka akitaka jengo la CCM liobomolewe ili kumpisha 'mwekezaji' 

Kwa vile kauli zifuatazo  “Nashawishika kuamini ukweli huu” na  “Nimependa uchambuzi huu wa sakata la Escrow, soma hapa” zikihusiana na makala “Sayansi ya hoja na mantiki katika Escrow Account” ni zako (Mwitumba), mimi nakwazika kidogo, na kama nitakuwa nimekukwaza wewe pia kwa mchango wangu basi naomba uniwie radhi.
Nakwazika kwa sababu wewe ni mwandishi mahiri na mhariri mkongwe uliyepata kuongoza gazeti la habari za uchunguzi la This Day, ina maana michezo iliyotumika katika kutengeneza makala ile kwa ngazi yako wewe, uzoefu na uelewa ni sawa na mtoto wa chekechea kumfundisha profesa taaluma yake!
Maneno “NASHAWISHIKA KUAMINI UKWELI HUU???!” badala ya “NASHAWISHIKA KUAMINI MAONI/UCHAMBUZI HUU” kidogo yanakwaza hasa yanapotoka katika fikra pevu za mwana taaluma mkongwe kama wewe. Hivi mpaka sasa bado unaamini kwamba kuna ukweli wowote katika sakata la Tegeta Escrow?
Unazungumzia ukweli upi? Ule unaoetetewa na Rais Kikwete, na timu yake ya akina Prof Muhongo? Eliakim Maswi, Prof Tibaijuka n.k. je ulisoma alichokieleza Prof. Benno Ndulu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania? Je umeyasoma majina ya wahusika wengine waliochota pesa hizo kama walivyoandikwa katika toleo moja la gazeti la Jamhuri?
Kisha nairejea kauli yako nyingine: “Nimependa uchambuzi huu wa sakata la Escrow, soma hapa” hivi hapo kuna uchambuzi kweli ndugu yangu Mwitumba? Mimi binafsi nimeona pumba tupu zilizoandikwa na waandishi ‘mamluki’ yaani wa kukodiwa ‘hack writers’ au ‘mercenary journalists’ watu ambao hulipwa pesa na kuandika upumbavu wowote wanaoelekezwa na mlipaji wao.

Nilitegemea kwamba kwa kuwa wewe umekaa kwenye chumba cha habari kwa muda mrefu kuliko mimi ambaye kwa muda mwingi nimekuwa nikiandika kama mwandishi wa kujitegemea na nimekaa katika chumba cha habari kwa muda usiozidi miaka sita (6) mpaka sasa, ungekuwa na upeo mkubwa zaidi wa kuunganisha mambo kulikoni mimi.
Kisha nataka nirejee katika jina la mwandishi mwenyewe anayeitwa KAZI MSEMAKWELI, binafsi katika taaluma yangu ya utambuzi wa majina niliyoipata wakati nikiwa Afisa Uhamiaji, hata jina lenyewe tu lina utata na linaacha maswali mengi kuliko majibu!. Mwandishi huyo ukiangalia jinsi alivyojenga hoja kwa hali yoyote ile ni mwandishi mkongwe.
Lakini ukienda kwenye facebook mtafute kwa jina hilo hapatikani, nenda tumia google search hapatikani, basi tafuta hata picha yake tu, haipatikani!. Ni dhahiri huyo ni mwandishi ‘ruhani’ ni mwandishi wa kutunga ‘fictitious’ au ni mwandishi jinni kitaaluma anakaribiana mno na hao ‘ghost writers’ ambao kazi yao ni kuandika fikra za watu wengine na wala siyo fikra zao wenyewe.


Ofisi ya jengo la CCM-Gama Makaani kabla halijabomolewa 


Ukiachana na jina lake nenda hata katika gazeti au magazeti ilipotumika makala hiyo, nimeisoma makala hiyo nzima yenye kurasa tatu na imeelezwa kwamba ilitumika kwa mara ya kwanza katika gazeti la Alhuda na ndipo ikahamishiwa katika gazeti la Taifa Imara.
Kimsingi magazeti haya yote mawili yamo katika mfumo wa umiliki unaoitwa ‘Quasi-independent’ kwa maana ya kwamba si magazeti huru bali ni magazeti huru nusu nusu! Kabla ya makala hii, gazeti la Taifa Imara liliwahi pia kuandika kwa “Wakatoliki wakerwa kwa maaskofu wao kudhaliishwa” uandishi wa ain hii mimi naona kwamba ni upuuzi mtu!
Ukitaka kuyafahamu kwa vile wewe ni mtaalamu basi fanya utafiti mdogo wa ‘content analysis’ rejea magazeti ya aina hii yaliandika nini kwa wakati wa uchaguzi wa mwaka 2010! Kwa mfano An-Nuur, Tazama Tanzania, Sauti ya Umma, na hata Changamoto yalijikita katika kuandika kwamba Dkt Slaa katumwa na Kanisa katoliki, kapora mke wa mtu, na hata kuunga mkono pale Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) lilipotoa vitisho.



Tayari jengo limeishapigwa nyundo kwa amri ya Tibaijuka na zoezi hilo kusimamiwa na Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bw. Ahmed Kipozi 
Magazeti mengine yaliyounga mkono habari hizo vikiwamo vitisho vya JWTZ ni Daily News, Uhuru, Jambo Leo, Habari Leo, An-Nur etc. uwiano wa sera kati ya magazeti haya na yale ya serikali na chama cha Mapinduzi ni kiashiria tosha kwamba hayo siyo magazeti huru bali yanafadhiriwa na watawala wetu wa sasa.
Natoa mifano michache: Tazama Tanzania Na.417, Oktoba 30, 2010 “Sababu za kutomchagua Dk Slaa kesho hizi hapa” Tazama Tanzania Na. 419, Nov 9-15, 2010 “kwa nini Kanisa Katoliki linataka kutupokonya Nyerere wetu?” An-Nuur 912, Septemba 28, 2010 “Tuhuma za uporaji wake za watu zitazamwe,”  na katika toleo hilo hilo: “Kikwete kawakosea nini maaskofu”
Ann Nur, Toleo Na. 903, Septemba 17-20, 2010 “CHADEMA ya walokole, akina Zitto mamluki?” Pia katika toleo hilo hilo “Slaa ni chaguo la Katoliki” An-Nuur Na. 903, Agosti 20-26, 2010 “Padri anaweza kuwa mtawala bora”
Mifano ipo mingi naomba nisiende zaidi katika hilo. Kuhusu gazeti la Taifa Imara ambalo mimi naamini bado ni jipya, ni miongoni mwa magazeti hayo hayo niliyoyazungumzia ambayo ni nusu huru, na yanalipwa na watawala wetu na kwa hiyo habari zake haziwezi kuaminiwa na watu makini aina ya Bw. Evarist Mwitumba.
Kuhusu migao ya pesa za Tegeta Escrow, kila mfuatiliaji makini atagundua kwamba huu ni muendelezo wa sakata la EPA, kwa sababu baadhi ya wanufaika wa pesa za EPA sasa tena ni wanufaika wa hizo za Escrow! Nani asiyefahamu kwamba Jaji Mujulizi alitokea katika kampuni ya mawakili ya IMMMA Advocates ambao walinufaika na pesa za EPA, mazingira ya uteuzi yake ni yapi, ni kwanini tena jaji huyu yumo kwenye mgao wa Escrow?
Kama pesa hizo ni halali mbona aina ya mgao uliofanyika unafuata mkondo yote ya fedha chafu zilizotakatishwa? Mbona Askofu Kilaini ni kiongozi pekee wa Kanisa Katoliki aliyepata kusema kuwa ‘Bw. Mafuta Mengi’  kwa kuazima msemo wa Wakenya ni chaguo la Mungu na sasa anapata mgao wa Escrow?
Ni nani asiyefahamu ubia wa Prof. Tibaijuka a.k.a jembe na ‘Bw Mafuta Mengi’ katika uporaji mkubwa wa ardhi? Mfano halisi ni jinsi alivyolazimisha kugawa ardhi kwa kampuni ya “mwekezaji bandia” ya Eco-Energy katika maeneo ya Bagamoyo?
Kwa mfano mimi nilipofuatilia katika Idara ya Uhamiaji makao makuu afisa wa vibali vya makazi akaniletea mafaili matano ambapo mwekezaji huyo amechukua ardhi kubwa, ambayo hata hivyo haifanyiwi kazi yoyote zaidi ya kuwapora wakulima wanyonge.
Nilipomhoji je ni kwa nini mwekezaji huyo anaishi Tanzania kuanzia mwaka 2007 mpaka mwaka huo (2014) bila kazi yoyote ki-Uhamiaji tunamuita ni mkazi mzigo (destitute) na serikali haijachukua hatua yoyote?


Wanakijiji wa Gama Makaani wakilalimikia kitendo cha kuporwa ardhi yao na kukabidhiwa mwekezaji wa ECO-ENERGY

Afisa huyo wa uhamiaji akanijibu “Bw. Elias, ndugu yangu, naomba achana na jambo hili, Tanzania ya leo siyo ya jana, unaweza kustukia mtu anakuchoma kisu chenye sumu kali mgongoni mwako na ukapoteza maisha yako, na muuaji asipatikane!, tulia tulee watoto ndugu yangu!” mwisho wa kumnukuu.
Kwa tafsiri yangu mwekezaji wa Eco-Energy ni muajiriwa wa Mtanzania tajiri na mwenye mamlaka (kama ilivyokuwa kwa IPTL, rejea kauli ya Mhe. Tundu Lissu kabla hajingiliwa na ‘Dr’ Mary Nagu, na ndiyo  maana anaweza kuishi nchini bila usumbufu na adha zozote toka Idara ya Uhamiaji.
Binafsi nimefanya mahojiano na Mkurugenzi Mkuu wa Eco-Energy Bw. Anders Bergfors ofisini kwake na pia Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Bw. Ahmed Kipozi na wote walijikanyaga tu katika majibu yao. Kwa hiyo Prof Tibaijuka alikuwa analipwa ujira wake kwa kufanikisha uporaji mkubwa wa ardhi haijalishi pesa hizo zilipitia miononi mwa nani iwe Rugemalira au Ruge-maliza!
Askofu Kilaini vivyo hivyo alikuwa anapata mgao wa shukrani kwa kusimama hadharani na kumfanyia mwanasiasa kampeni kinyume na msimamo wa kanisa lake. Viongozi wengine kama Askofu Nzigilwa na mapadri wanaweza kuwa wametumika tu ili kuficha lengo hatuwezi jua labda wanaandaliwa kwa ajili ya kusaidia kampeni za 2015.
Prof. Muhongo anafahamika kwa ubabe wake wa kukataa kutoa mikataba katika sekta ya mafuta na gesi asilia kama sheria na mikataba ya kimataifa inavyotakiwa yaani kuwa ya wazi badala kuwa mali na siri ya serikali pekee.
Rejea vipengele hivyo katika African Peer Review Mechanism (APRM) na Open Government Partneship (OGP) inavyoagiza. Kuhusu utakatishaji wa fedha ni somo ninalolifahamu kwa kina.
Nilipata mafunzo juu ya utakatishaji wa pesa kutoka taasisi ya kupambana na utoroshaji wa watoto, yaani African Network for The Prevention & Protection against Child Abuse and Neglect (ANPPCAN) na mpango wa kupambana na ufadhili kwa ugaidi na uhalifu mwingine mkubwa.
Pia nimewahi kupata mafunzo mengine kama hayo kutoka kwa taasisi ya Financial Transparency Coalition, chini ya asasi ya Policy Forum.

kadi ya utambulisho katika mafunzo ya uhalifu kuhusiana na fedha, kukwepa kodi na kutakatisha fedha yaliyodhaminiwa na asasi ya Policy Forum 

Hivyo basi kilichofanyika katika benki za Mkombozi na Stanbic ndiyo hicho hicho hufanyika katika utakatishaji wa pesa chafu za kiharamia je ni kwa nini iwe hivyo? Yaani akaunti inafunguliwa, pesa zinawekwa na kuchotwa kisha akaunti inafungwa! Bado kuna utetezi hapo jamani? Je kweli hiyo ni pesa safi? Kwa nini iondolewe katika njia chafu? Njia za hofu hofu?
Unaweza kusoma kitabu cha Paul Allan Schott: Reference Guide to Anti-Money Laundering and Combating the Financing of Terrorism, kwa uelewa zaidi kipate hapa: http://siteresources.worldbank.org/EXTAML/Resources/3965111146581427871/Reference_Guide_AMLCFT_2ndSupplement.pdf
Hitimisho
Naamini wasomaji watapata mwanga ni kwa nini maprofesa hao ‘majembe’ wamekuwa na viburi na kujiamini sana ni kwa sababu wanajiona kwamba wao wazijua siri za ‘wakubwa’ kwa undani zaidi, yaani Muhongo katika suala la mikataba ya mafuta na gesi asilia na Tibaijuka kuhusu uporaji mkubwa wa ardhi sehemu mbali mbali za nchii (rejea lugha ya tulimuita, tukazungumza tukamuomba…)

MUNGU IBARIKI AFRIKA, MUNGU UBARIKI TANZANIA 
Mwandishi wa uchambuzi huu ni mkurugenzi wa utafiti na uchunguzi kutoka chama cha waandishi wa habari za haki za binadamu-JOURNORIGHTS